Sunday, August 17, 2014

Hoja mpya zalichanganya Bunge Maalumu

By on 12:04 AM
Mwenyekiti wa Kamati Nambari 10 wa Bunge Maalumu la Katiba, Salmin Awadh Salmin akizungumza na waandishi wa habari Dodoma jana. Picha na Emmanuel Herman 
Na Waandishi Wetu, Mwananchi

  • Ni kuhusu muundo wa taasisi muhimu, Bunge, Mahakama  na nafasi za juu za uongozi
  • Sumaye ashauri Mchakato wa Katiba usimamishwe, maridhiano yafanyike


Dodoma. Mapendekezo mapya yanayopelekwa kwenye Kamati za Bunge Maalumu kwa ajili ya kurekebisha baadhi ya Ibara za Rasimu ya Katiba, yamezua mivutano mikali kiasi cha baadhi ya sura kuwekwa kiporo au kurukwa na kamati husika.
Habari zilizolifikia gazeti hili zinasema mapendekezo hayo ni yale yanayozigusa taasisi kubwa za nchi, zikiwamo Bunge la Jamhuri ya Muungano na Mahakama, pamoja na nafasi za Makamu wa Rais.
Katika baadhi ya kamati yamepelekwa mapendekezo ambayo yanataka Bunge liwe na sehemu tatu ili kutoa fursa kwa mambo ya Tanzania Bara kujadiliwa bila wabunge kutoka Zanzibar kuwapo.
“Mapendekezo yaliyopo ni kwamba wanataka Bunge liwe na sehemu tatu ambazo ni Bunge la Muungano kwa masuala ya muungano na humohumo linakuwa na sehemu mbili ambazo ni wabunge wa Zanzibar kwa ajili ya masuala ya Wazanzibari na sehemu ya Tanganyika kwa ajili ya mambo ya bara,” kilisema chanzo chetu kutoka katika kamati moja ya Bunge hilo.
Hata hivyo, habari zinasema baadhi ya wajumbe wa kamati walikosoa pendekezo hilo kwa maelezo kwamba linashabihiana na muundo wa muungano wa serikali tatu ambao ulipendekezwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba lakini ukapingwa na baadhi ya wajumbe wakiongozwa na walio wanachama wa CCM.
Jana Mwenyekiti wa Kamati Namba 8, Job Ndugai aliwaambia waandishi wa habari kwamba kamati yake imeshindwa kuafikiana kuhusu muundo wa Bunge la Muungano hivyo kulazimika kuliacha suala hilo ili kulifanyia uchunguzi kwanza.
“Mbali na sura ya 5 inayozungumzia uraia pacha ambayo ilitusumbua, lakini pia suala la Muundo wa Bunge la Muungano na Mahakama ya Muungano vilikuwa tatizo katika kamati yangu,” alisema Ndugai.
Licha ya kwamba Ndugai hakuzungumzia suala hilo kwa undani, lakini taarifa zilizolifikia gazeti hili zinasema muundo wa kuwa na sehemu tatu katika Bunge moja ndio uliozua mtafaruku kiasi cha kamati hiyo kuliahirisha.
Katika kamati namba 5, sura ya 10 inayozungumzia suala la Bunge na Mahakama imerukwa. Mmoja wa wajumbe wa kamati hiyo alisema: “Tumeamua kuendelea na mambo mengine kwanza maana hilo limeonekana kuwa ni gumu kwa sasa.”
Habari zaidi zinasema katika kamati hiyo namba tano, mapendekezo ya kuwapo kwa makamu wa rais watatu yalizua mjadala mkali kiasi cha kusababisha kuwapo kwa wajumbe walioamua kuandaa maoni ya wachache.
“Wamekuja na mapendekezo kwamba awepo Makamu wa Kwanza wa Rais ambaye atakuwa mgombea mwenza, Makamu wa Pili wa Rais ambaye atakuwa Rais wa Zanzibar na Makamu wa Tatu wa Rais ambaye ni Waziri Mkuu,” kilisema chanzo chetu kutoka ndani ya kamati hiyo na kuongeza:
“Lakini wapo waliokataa kama watano au sita hivi na wameamua kwamba wataandika maoni ya wachache kwa mujibu wa Kanuni ya 32 (10)”.

0 comments:

Post a Comment