Friday, August 15, 2014

Ugonjwa wa EBOLA Waingia Dar es Salaam……Wagonjwa wawili wagundulika kuwa nao

By on 9:06 AM

Ugonjwa wa Ebola umeingia nchini kufuatia watu wawili wanaodhaniwa kuwa na maambukizi yake kuwasili nchini.
 
‘Wagonjwa’ hao wamepelekwa katika kituo maalum kilichotengenezwa na serikali kwa ajili ya waathirika wa ugonjwa huo kilichopo wilaya ya Temeke jijini Dar es Salaam.
 
Mpekuzi jana ilishuhudia watu wawili wanaodhaniwa kuwa na ugonjwa huo wakiwa wamefikishwa katika kituo hicho maalum, mmoja akitokea katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA).
 
Mmojawapo anayedaiwa kuwa ni raia wa Benin, kabla ya kufikishwa kwenye kituo hicho alipitia katika Hospitali ya AMI iliyopo jijini Dar es Salaam.
 
Wakati mgonjwa wa Benin akifikishwa kituoni hapo, mwingine alifikishwa kituoni hapo huku akitokwa na damu puani zilizokuwa  zimezibwa kwa pamba.
ebola
 
Mwandishi alizungumza na Kaimu Mganga Mkuu wa Dar es Salaam, Dk. Grace Maghembe, ambaye alisema alikuwa ‘bize’ kuwashughulikia hao wagonjwa na kuomba apigiwe simu baada ya saa moja.
 
“Nipo kuna kitu nafanya. Hebu nipigie baada ya saa moja kwa maana nashughulikia wagonjwa hao hao,” alisema na kukata simu huku akionekana kutingwa na jambo kubwa.

Baada ya saa moja Mwandishi alizungumza na Dk. Maghembe ambaye alithibitisha kuwapo kwa wagonjwa wawili, mmoja raia wa Benin na mwingine Mtanzania.
 
Mwandishi pia lilishuhudia harakati za kuandaa eneo la kupokea wagonjwa wa ugonjwa huo eneo la Temeke ambako hadi sasa ni watu hao wawili wanaohofiwa kuwa wagonjwa wa kwanza kutambuliwa nchini.
 
Wakati Tanzania ikivamiwa na janga hilo, Shirika la Afya Duniani (WHO) jana lilitahadharisha kuwa Kenya inaweza kuwa katika hatari ya kukumbwa na ugonjwa huo kutokana na kasi ya kuenea kwake Barani Afrika.
 
Hofu hiyo inaelezwa kutokana na Kenya kuwa kitovu cha usafiri wa ndege kwa nchi za Afrika Mashariki na Kati huku wasafiri wengi wanaokwenda na kurudi kutoka nchi za Afrika Magharibi wakipitia jijini Nairobi.
 
Taarifa hiyo iliyokaririwa na Shirika la Utangaza la Uingereza (BBC), WHO imetoa onyo hilo ili nchi za ukanda wa Afrika Mashariki zijipange kukabiliana na hati ya mlipuko wa Ebola.
 
Hali hiyo inatokea wakati wataalamu wa afya wanasema kwamba wanajitahidi kudhibiti mlipuko wa ugonjwa huo Afrika Magharibi, ambako zaidi ya watu 1,000 wameripotiwa kufa kutokana na ugonjwa huo.
 
Canada imesema kwamba itatoa mchango wa dozi 1000 za chanjo ya majaribio ya Ebola kusaidia watu kutoambaukizwa ugonjwa huo.
 
Mgonjwa wa kwanza  wa Ebola, aliripotiwa nchini Guinea Februari mwaka huu kabla ya kuenea hadi Sierra Leone na Liberia.
 
Nigeria imekuwa mwathirika mkubwa wa ugonjwa huo hasa kutokana na kuwa na idadi kubwa ya watu barani Afrika ikiwa na misongamano mingi ya watu na inakadiriwa kuwa takribani theluthi moja ya vifo vya Ebola vimetokea nchini humo.
 
EBOLA NI UGONJWA GANI?
Ugonjwa wa Ebola unaenea kwa kasi kwa kuambukizwa na kirusi kinachopatikana katika ukanda wa nchi za joto.
 
Dalili za ugonjwa huo ni homa kali ya ghafla, kulegea mwili, maumivu ya misuli, kuumwa kichwa na vidonda kooni.
 
Mara nyingi dalili hizo hufuatiwa na kutapika, kuharisha, vipele vya ngozi, figo na ini kushindwa kufanyakazi na kwa baadhi ya wagonjwa kutoka damu ndani na nje ya mwili.

0 comments:

Post a Comment