Monday, July 7, 2014

CUF NAO WAFUNGUKA KUHUSU URAIS NA UJANA

By on 5:10 AM


VIJANA wanaotaka uongozi hususani nafasi ya urais, wameshauriwa kujenga hoja, kuonesha malezi mazuri waliyo nayo na karama ya uongozi, ili watu wabaini wawachague, badala ya kuegemea kigezo cha rika kuwapatia nafasi husika.
Imeelezwa katika uchaguzi mkuu ujao, vyama vingi vinaweza kusimamisha wagombea vijana kwa kuzingatia hoja inayotawala, ikageuka kete ya kupandisha chama chati, lakini kwa upande wa kiongozi, akawa asiyefaa.
Wanasiasa kutoka vyama vya siasa tofauti, walisema hayo juzi kwenye kipindi kilichokuwa kikirushwa moja kwa moja na televisheni ya Star chini ya mada iliyosema, ‘Vijana na Kasi ya Kushika Madaraka; Je 2015 ni wakati wao?’
Naibu Mkurugenzi, Mawasiliano wa Chama cha Wananchi (CUF), Abdul Kambaya alisema kama vigezo vya kupata kiongozi vikianza kuwa kutaka kuongozwa na kijana, nchi inaweza kuongozwa na mtu asiyefaa.
Kambaya alitoa mfano wa Jaji Joseph Warioba, aliyetoa ushauri kwamba ni vyema vijana washike hatamu, na kusema licha ya kwamba ni mzee, alipopewa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, aliiongoza vizuri .
Kiongozi huyo wa CUF alisema, hekima, busara ya uongozi siyo tu inatokana na maandalizi, bali pia na kipaji ambacho ni zawadi kutoka kwa Mungu.
Alisisitiza kwamba matatizo ya Watanzania hayatokani na wazee, isipokuwa ni ya kimfumo kwa maana kwamba hata kijana akiingia madarakani bila mfumo kubadilika, yataendelea kuwepo.
“Uzee siyo ugonjwa na ujana si dawa ya matatizo tuliyokuwa nayo. Tatizo ni la kimfumo. Hata aje kijana, mfumo tulio nao ndiyo utaendelea…ujana hauwezi kuwa kete,” alisema Kambaya na kutolewa mfano wa baadhi ya taasisi serikalini zinazoongozwa na zilizowahi kuongozwa na vijana lakini zikafanya vibaya.
Kambaya alisema upo uwezekano mkubwa wa vyama vingi vya siasa, kusimamisha mgombea kijana kwa kuzingatia hoja hiyo inayotawala na inayojaribu kuaminisha jamii kwamba vijana ndiyo wanapaswa kupewa nafasi.
Alisema, “inawezekana vyama vingi vikasimamisha vijana kwa kuzingatia hoja inayotawla. Lakini hiyo itakuwa ni kupandisha vyama. Vitapata Rais lakini anaelewa matatizo au ni tamaa ya kupata mali?.” Kiongozi huyo wa chama aliendelea kusisitiza haja ya kutochagua rais kwa sababu ya ujana wake.”Suala ni vigezo. Tukipiga chapuo ya vijana na wazee, hatutaondoa matatizo yaliyopo.”
Kwa upande wake, mwanasiasa mkongwe na kada wa Chama Cha Mapinduzi, Emmanuel Rutaraka, alisema ni vigumu kuwaengua wazee katika uongozi, huku akisisitiza kiongozi ni lazima aandaliwe.
Akisisitiza dhana ya kuandaliwa, mwanasiasa huyo alitoa mfano wa Rais Jakaya Kikwete na kusema alianza kuandaliwa tangu awali. Alisema wakati Mwalimu Julius Nyerere akipigania uhuru, aliungwa mkono na wazee.
“Vijana wakubali kuandaliwa..ukisema wazee wakae kando, nani ataandaa vijana,” alihoji Rutaraka aliyewahi kuwa Mbunge wa Bukoba Mjini takribani miaka 30 iliyopita.
Mwanasiasa huyo mkongwe alikemea vijana wanaoponda wazee kwamba wamepitwa na wakati, akisema, “hicho ni kiburi na ubinafsi kuwaambia wazee wamepitwa na wakati.”
Alishauri vijana wanaotaka uongozi hususani nafasi ya urais, wajenge hoja, waoneshe malezi mazuri na karama ili watu wakibaini hayo, wawachague na siyo kutanguliza kigezo cha umri
                             <<BOFYA ULIKE PAGE KWA HABARI ZAIDI>>

0 comments:

Post a Comment