Wednesday, July 9, 2014

SOMA KISA HAPA:BABU MIAKA 82 AUAWA KWA KUVUNJWA SHINGO...

By on 2:32 AM
Stori ya kifo cha mzee Halfan Mohammed Mtonga (82) mkazi wa Kijiji cha Pela, Chalinze, Wilaya ya Bagamoyo mkoani hapa kinachodaiwa kutokana na kuvunjwa shingo, inasikitisha.
Marehemu mzee Halfan Mohammed Mtonga (82) mkazi wa Kijiji cha Pela, Chalinze, Wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani akisindikizwa katika safari yake ya mwisho.
Tukio hilo lilitokea Julai 3, mwaka huu nyumbani kwake baada ya kuzidiwa, hali yake ilipobadilika siku kadhaa tangu aliporuhusiwa hospitalini.
Akisimulia tukio zima kwa majonzi, mjane wa marehemu Aisha Amir (75) alisema, ameumia sana kumpoteza mume wake kipenzi ambaye anadai kukatishwa uhai na mpwa wake aliyemtaja kwa jina moja la Sabata aliyemshambulia na kumvunja shingo.

“Siku ya tukio tulikuwa tumelala mimi na mume wangu, ghafla tukaona mwanga wa tochi, tulipofuatilia tukagundua ni Sabata, nilipomwambia anataka nini, akatishia kuniua. Alisema nikae kimya.
“Alimwamrisha marehemu aamke ili ampe chipsi na soda alizomletea lakini alikataa kutokana na hali yake kiafya kuwa mbaya. Alipoona amekataa, alimsukuma chini kwa nguvu, mzee akaanza kulia akilalamikia maumivu makali ya shingo. Tukiwa tumeduwaa, Sabata alianza kumwagia haja ndogo usoni,” alisema Bi. Aisha akimwaga machozi.

Marehemu mzee Halfan Mohammed Mtonga enzi za uhai wake.
Alisema baada ya tukio hilo, majirani waliitana kisha kumkimbiza hospitalini kwa matibabu ambapo uchunguzi ulionyesha kuwa alivunjika shingo.
“Hata hivyo alifanyiwa matibabu na kuruhusiwa, akaonekana kuwa na hali ya kuridhisha kabisa, hadi hali yake ilipobadilika nyumbani na kufariki,” alisema Bi. Aisha.
Naye mtoto wa marehemu, Seleman Halfan alisema muda mfupi kabla ya baba yake kufariki, alikuwa akilalamika kuuawa na mpwa wake Sabata.

“Mzee wangu amekufa kifo kibaya sana, sijui ni kwa nini huyo Sabata alifikia hatua hiyo. Kila wakati alikuwa anasema; Sabata unaniua, Sabata unaniua! Yaani ametuacha na maswali mengi sana. Lakini tunaamini sheria itafuata mkondo wake,” alisema Seleman.
Mtuhumiwa huyo alikamatwa na kufikishwa katika Kituo cha Polisi Chalinze kisha kupelekwa mahabusu katika Gereza la Mifugo la Ubena, Chalinze mkoani hapa akisubiri hatua zaidi za kisheria.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, SACP Nesphory Matei alithibitisha kutokea kwa tukio hilo ambapo aliwataka wananchi kutoa taarifa kwa vyombo vya dola dhidi ya watu wasio wema kwenye jamii.

0 comments:

Post a Comment